Kasi ya maendeleo katika nchi zinazoendelea inaweza kurudi nyuma miaka mitano
ijayo, iwapo hatua thabiti hazitachukuliwa kupunguza kasi ya mabadiliko ya hali
ya hewa.
Ripoti ya 2011 kuhusu
Uendelevu na Usawa ilieleza kuwa, uendelevu wa mazingira unaweza kufikiwa kwa
njia ya haki na yenye matokeo mema iwapo masuala ya afya, elimu, kipato na
tofauti za jinsia kuchukuliwa hatua za kimataifa kuhusu uzalishaji.
Uharibifu wa mazingira
unatishia uhai wa viumbe duniani kwa kiasi kikubwa hutokana na shughuli
mbalimbali za wanadamu ikiwemo ukataji miti na kuchoma moto misitu ya asili.
Msisitizo mkubwa umekuwa
ukifanywa na wadau wa mazingira kwa kuhakikisha mikataba na sheria zinawekwa
ili kulinda, mazingira na viumbe adimu wasitoweke.
Wilaya ya Kilombero ni
moja ya wilaya iliyobarikiwa kuwa na mito zaidi ya 20 kati yake mito mikubwa 9
isiyokauka maji kwa kipindi cha mwaka mzima Mbali na vivutio hivyo, kumekuwa na
uelewa mdogo wa masuala ya uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya maji .
Ukosefu wa elimu
katika vijiji mbalimbali ndani ya wilaya hiyo umesababisha wananchi kushindwa
kutambua umuhimu wa kuhifadhi mazingira na vyanzo vya maji vilivyowazunguka
katika maeneo yao.
Tatizo la uharibifu wa
mazingira na uchafuzi wa vyanzo vya maji ni baadhi ya sababu kubwa
zinazochangia upungufu wa maji na mabadiliko ya tabia nchi .
Ongezeko la watu na
kukua kwa shughuli za kiuchumi pia, ni chanzo cha ongezeko la matukio ya
uchafuzi wa mazingira na vyanzo vya maji katika maeneo hayo.
Hivi karibuni katika
Kijiji cha Sanje Tarafa ya Kidatu, Wilaya ya Kilombero, kulikuwa na mgogoro wa
wananchi na kufikia hatua ya kuziba barabara kuzuia magari yaendayo makao makuu
ya wilaya hiyo kupitika kwa urahisi baada ya mwenyekiti wa kijiji hicho na
wajumbe wawili kufikishwa mahakamani kwa tuhuma za kuharibu vyanzo vya maji .
Mabadiliko ya tabia
nchi yamekuwa yakiathiri kwa kiasi shughuli za maendeleo hasa katika sekta ya
kilimo , kutokana na mfumo wa wakulima nchini kutegemea mvua za masika.
Mwenyekiti huyo hakusita
kueleza ukweli katika suala zima la tuhuma zinazowakabili mpaka kufikia kuingia
hatiani kuwa ukosefu wa elimu juu ya masuala ya uhifadhi wa mazingira , ardhi
na vyanzo vya maji kwa viongozi katika Serikali za mitaa .
Mwenyekiti huyo
alikiri kutenda kosa hilo kwa kisingizio cha kukosa elimu kuhusu uhifadhi wa
mazingira, vyanzo vya maji na ardhi.Ofisa wanyamapori Wilaya ya Kilombero, Bw.
Madaraka Aman anasema kuwa, uongozi wa serikali ya kijiji hicho ulichepusha mto
Sanje kwa lengo la kutaka kujinufaisha wenyewe badala ya manufaa kwa wananchi .
Anasema, azimio la
mwaka 1970 la mkutano uliofanyika katika mji mdogo nchini Iran unaotambulika
uliweka mikataba ya kuhifadhi ardhi oevu kwa lengo la kulinda, mito, mazingira
na vyanzo vya maji.
Mkataba huo
unatahadharisha na kutaka udhibiti wa mambo yanayohatarisha uharibifu wa
mazingira kama kuziba mito, kuchepusha mito, kukausha, kuchimba mawe katika
vyanzo vya maji pia, shughuli zote zenye kuhatarisha mazingira .
Anasema, sheria
hiyo inapaswa kuzingatiwa na idara za Serikali ikiwa ni pamoja na mamlaka za
maji , ambapo katika sheria hiyo kifungu cha 8 kinatamka kuwa ‚"maji yote
yaliyopo Tanzania ni mali ya jamhuri ya muungano,".
Kwa mujibu wa
sheria hiyo maji ni rasilimali ya taifa ,hakuna umiliki binafsi wa rasilimali
za maji hata kama yapo au yanapita katika eneo la makazi ya watu.
Anasema, mtu
ama taasisi anaweza kupewa haki ya kutumia na sio kumiliki ambapo, haki hiyo
hutolewa na ofisi za mabande tu hivyo kwa misingi hiyo uongozi wa Serikali ya
kijiji ulifanya kosa kwa kujua ama kutojua sheria .
Anasema kuwa,
sheria hiyo inasema baadhi ya miradi haitaruhusiwa kutekelezwa kabla ya
kufanywa tathmini ya uharibifu wa mazingira.Anaeleza kuwa, adhabu ya kosa hilo
ni kuwa mtuhumiwa yeyote atakayeingia hatiani kwa makosa ya sheria hiyo atapewa
adhabu ya faini kiasi cha shilingi 50,000 mpaka milioni 50 ama kifungo cha
kuanzia miaka mitatu mpaka saba .
Kifungu hicho
kitamhusu mtu ambaye atakiuka kifungu cha sheria namba 57 ya mazingira bila
kujali nyadhifa yake ndani ya Serikali au chama Hata hivyo Bw.Madaraka anadai
kuwa sekta ya maliasili imekuwa ikikwamishwa kutekeleza baadhi ya majukumu
kutokana na kuingiliana na masuala ya kisiasa wanapokuwa wakitekeleza majukumu
yao kwa mujibu wa sheria na taratibu za kazi.
Anadai kuwa,
baadhi ya wanasiasa wamekuwa chanzo kikubwa cha uharibifu wa mazingira katika
maeneo yao, kwa kuona nafasi zao za kisiasa katika uvunjwaji wa sheria katika
idara ya maliasili .
Anasema, kesi
nyingi za maliasili itikadi za kisiasa zimekuwa zikiingia na hivyo kuwafanya
wataalamu wa idara hiyo kushindwa kutekeleza wajibu wao .Amewataka viongozi wa
kisiasa, kutoingilia shughuli na utekelezaji wa udhibiti wa matukio ya
uharibifu wa mazingira na badala yake waendelee kufanya shughuli zao.
"Wanasiasa
wamekuwa kikwazo katika kutekeleza majukumu yetu kwa mujibu wa sheria"
anasema Bw. Madaraka.Anasema, majukwaa ya kisiasa yanatakiwa kutumika
kuelimisha wananchi juu ya umuhimu wa kutunza na kuhifadhi mazingira katika maeneo
yao, badala ya kuwapotosha pale wanapoingia hatiani na kuwashawishi kufanya
maandamano yasiyo na msingi.