Wednesday 26 February 2014

MIKONO YA WANASIASA INAVYOCHOCHEA MIGOGORO YA ARDHI



Dar es Salaam. Migogoro ya ardhi inayojitokeza kwa sasa katika jamii imeendelea kuwa tishio la amani ya nchi yetu kutokana na athari mbalimbali zinazodaiwa kuchangiwa na matokeo ya udhaifu wa kimfumo, ongezeko la idadi ya watu, shughuli za uwekezaji, upanuzi wa miji, shughuli za ufugaji na nyinginezo nyingi.
Athari hizo zimesababisha watu kupoteza makazi, mifugo na mauaji ya kikatili kutokana na vita kati ya wakulima na wafugaji, wanavijiji na wawekezaji na wengineo, wakigombania umilliki wa ardhi katika eneo moja.
Aidha, takwimu zinaonyesha kwamba kati ya hekta milioni 80 za ardhi ya kilimo nchini, ni asilimia 10 ndiyo iliyopimwa katikati ya ongezeko la Watanzania milioni 45.
Hatua hiyo inaweza kuwa sababu ya kuwapo kwa zaidi ya kesi 6,000 za migogoro ya ardhi zinazoendeshwa katika Mahakama Kuu ya Tanzania kote nchini.
Katika kushughulikia changamoto hiyo, Serikali kupitia Tume ya Kurekebisha Sheria ikaingia kwenye mchakato wa kuandaa ripoti inayohusu migogoro ya ardhi nchini ili kutoa nafasi ya kufanyiwa marekebisho Sheria ya Ardhi huku ikiwashirikisha wadau wote ikiwamo, mahakama, Wizara ya Ardhi, wananchi na wanasheria.
Jaji Mkuu, Mohamed Othman Chande anasema ili kumaliza migogoro hiyo nchini kwa sasa ni lazima kila kesi husika iangaliwe msingi wake kwa kuzingatia inapatikana katika ngazi gani kwani migogoro mingi ipo katika ngazi za chini.
Hata hivyo, wakati harakati hizo zikiendelea, wanasiasa wamekuwa wakionekana kuingilia kati migogoro hiyo huku wakituhumiwa kulinda masilahi yao kisiasa pasipo kujali hatima ya wananchi ambao wamekuwa wakiendelea kuathirika zaidi.
Ofisa Mradi wa Haki Ardhi, Cuthbert Tomito anasema wanasiasa, hususan wabunge waliozungukwa na migogoro ya ardhi wamekuwa wakipotosha wananchi, hatua ambayo inasababisha kuchochea machafuko.
“Katika hatua za kutatua migogoro kuna mambo yanayoamuliwa kitaalamu, wakati mwingine wananchi wanaweza kuwa na makosa lakini wanasiasa wanaingilia kati kuwalaghai, kuwatia moyo matokeo yake wananchi wanafikia hatua ya kukosa uvumilivu wakiamini wana haki kumbe sivyo,” anasema Tomito na kuongeza:
“Wanasiasa wanapokuwa tayari wameingilia migogoro hiyo, upande wa watendaji ambao ni maofisa ardhi wanakosa nguvu ya kutekeleza majukumu yao, kwa hivyo ningewashauri katika hatua za kushughulikia migogoro hiyo, ni vyema wakaachia watendaji kwani wao wanafanya kazi kwa mujibu wa sheria.”
Tomito anaongeza kuwa watendaji wanatakiwa kuachiwa nafasi yao wafanye kazi na wasiingiliwe kwa sababu sheria haina upindishwaji.
“Mtendaji ana uhuru mkubwa katika majukumu yake pengine tofauti na mwanasiasa ambaye anahofia kutofautiana mtazamo na wapigakura wake,” anasema.
 Source: Mwananchi

Friday 21 February 2014

UKRAINE: HATIMAYE MAKUBALIANO YAPATIKANA



Habari za hivi punde zinaarifu kuwa ofisi ya rais Yanukovych nchini Ukrain imetoa taarifa inayosema kwamba mwafaka umefikiwa katika mazungumzo ya usiku kucha kati ya serikali ,upinzani na waakilishi wa Muungano wa Ulaya na Urusi.


Katibu mkuu wa UN Ban Ki Moon amesema kuwa hali Ukraine ni ya kutamausha


Taarifa hiyo hata hivyo haikutoa maelezo zaidi kuhusu makubaliano hayo ingawa ilisema kuwa pande zote zitatia saini makubaliano yenyewe
Duru zinasema kuwa Rais Yanukovych amekuwa akikabiliwa na shinikizo apange uchaguzi wa mapema pamoja na mageuzi ya kikatiba.
Umoja wa Ulaya umekubali kuwawekea vikwazo viongozi waliopanga ghasia zinazoikabili Ukraine kwa sasa.
Uamuzi huo uliofanyika mjini Brussels, Ubelgiji umejiri baada ya watu kadhaa kuuawa mjini Kiev, katika siku ambayo ilishuhudia umwagikaji mkubwa zaidi wa damu tangu uhuru wa Ukraine zaidi ya miaka ishirini iliyopita.
Waziri wa mashauri ya nchi za kigeni wa Italia, Emma Bonino, amesema vikwazo hivyo vinavyojumuisha vya usafiri na kupiga tanji mali za wahusika na kwamba vinawalenga wale waliohusika na mauaji ya waandamanaji.
Ujumbe wa Umoja wa Ulaya mjini Kiev unajaribu kuwapatanisha viongozi wa upinzani na rais Victor Yanukovych ili kuleta amani na pia kushawishi taifa hilo kuandaa mapema uchaguzi uliopangiwa kufanyika mwaka ujao.
Katibu mkuu wa umoja wa mataifa , Ban Ki-moon amesema hali nchini Ukraine ni ya kutamausha:
Wito huo umetolewa vile vile na waziri wa mashauri ya nchi za kigeni wa Marekani John Kerry ambaye ametaka vurugu kusitishwa nchini Ukraine akisema kuwa watu wa taifa hilo wanastahili kuwa na hali bora kuliko kile alichokitaja kuwa maafa na mateso yasiyofaa ambayo yameshuhudiwa katika barabara za mji mkuu, Kiev.
Haijabainika ni watu wangapi waliouwawa katika vurugu za Alhamisi lakini wizara ya Afya inasema tangu Jumanne, watu sabini wameuawa na zaidi ya 570 wamejeruhiwa.
SOURCE: BBC-Swahili