Friday 8 July 2016

France Na Ureno fainali jumapili

Ufaransa imetinga katika hatua fainali ya Kombe la Mataifa barani Ulaya kwa mwaka huu baada ya kuifunga Ujerumani 2 - 0.
Mshambuliaji Antoine Griezmann ndiye aliyeipeleka timu yake ya Ufaransa katika hatua fainali ya Kombe la Mataifa barani Ulaya kwa mwaka huu baada ya kuifungia magoli 2 na kuishangaza Ujerumani iliyokuwa imetawala mchezo huo wa nusu fainali.

Mshambuliaji huyo wa Atletico Madrid alianza kwa kuandika bao la kwanza kwa njia ya penalti katika dakika ya 45 kipindi cha kwanza kabla ya kupachika bao la pili na ushindi kipindi cha pili baada ya golikipa wa Ujerumani Manuel Neuer kufanya makosa golini.
Kwa matokeo hayo sasa Ufaransa mwenyeji wa michuano hiyo itakutana na Ureno katika mechi ya fainali siku ya Jumapili

Friday 1 July 2016

Wakuu wa Wilaya na kasi ya maendeleo Tanzania

taarifa kwa vyombo vya habari
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
KURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU

Simu : +255-22-2114512, 2116898
Tovuti : www.ikulu.go.tz
Faksi : 255-22-2113425
OFISI YA RAIS,
IKULU,
1 BARABARA YA BARACK OBAMA,
11400 DAR ES SALAAM,
TANZANIA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 29 Juni, 2016 amewaapisha wakuu wa Mikoa watatu aliowateua Jumapili iliyopita tarehe 26 Juni, 2016.
Wakuu wa Mikoa walioapishwa leo Ikulu Jijini Dar es salaam ni Dkt. Binilith Satano Mahenge ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dkt. Charles Ogesa Mlingwa ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Mara na Bi. Zainab Rajab Telack ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.
Hafla ya kuapishwa kwa wakuu hao wa Mikoa imehudhuriwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama na wakuu wa wilaya wateule ambao waliteuliwa na Rais Magufuli Jumapili iliyopita tarehe 26 Juni, 2016.
Aidha, miongoni mwa wakuu wa wilaya 139 walioteuliwa, Rais Dkt. John Pombe Magufuli amefanya mabadiliko madogo katika wilaya tatu ambapo ametengua uteuzi wa Mkuu wa Wilaya ya Rombo Mteule Mhe. Fatma Hassan Toufiq na badala yake amemteua Bi. Agness Elias Hokororo kuwa Mkuu wa Wilaya hiyo, ametengua uteuzi wa Mkuu wa wilaya ya Serengeti Mteule Bw. Emile Yotham Ntakamulenga na badala yake amemteua Bw. Nurdin Hassan Babu kuwa Mkuu wa Wilaya hiyo na ametengua uteuzi wa Mkuu wa Wilaya ya Ikungi Mteule Bw. Fikiri Avias Said na badala yake amemteua Bw. Miraji Mtaturu kuwa Mkuu wa wilaya hiyo.
Akizungumza katika hafla hiyo, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewataka wakuu wa wilaya wateule kwenda kuchapa kazi na kutatua kero za wananchi katika wilaya zao huku wakizingatia kufanya kazi kwa uadilifu na uaminifu.
Rais Magufuli pia amewataka kusimamia ukusanyaji mapato ya serikali na matumizi ya fedha na rasilimali nyingine za umma, kuhakikisha wananchi wapo salama na pia kuhakikisha wananchi wanafanya kazi za uzalishaji mali.
"Katika kazi hizi wapo watakaowakejeli, katika kazi hizi wapo watakaowadhihaki, nyinyi kavumilieni na mmuweke Mungu mbele na mkawaweke watanzania mbele, mkafanye kazi kadiri Mungu atakavyokuwa amewaongoza.
"Nataka kuwahakikishia tunawaunga mkono kwa nguvu zote, mkafanye kazi bila uwoga wowote, katembeeni kifua mbele, kwa sababu tumewaamini wala msiwe na wasiwasi, ukifanya kitu kizuri kwa dhamira yako iliyo njema kitazaa matunda mazuri, ukifanya kitu kwa unafiki hakitafanikiwa" Amesema Rais Magufuli
Katika hafla hiyo, wakuu wa mikoa walioapishwa na wakuu wa wilaya wateule wamekula kiapo cha ahadi ya uadilifu kwa viongozi wa umma, zoezi ambalo limeongozwa na Kamishna wa Maadili Jaji Mstaafu Salome Kaganda.
Katika hatua nyingine, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amekutana na kufanya Mazungumzo na mwenyekiti mwenza wa taasisi ya Bill and Melinda Gates ya Marekani Bi. Melinda Gates ambapo Rais Magufuli amemuhakikishia mwenyekiti mwenza huyo kuwa serikali ya awamu ya tano itaendeleza na kuimarisha zaidi uhusiano wake na taasisi hiyo ambayo imekuwa ikishirikiana na Tanzania katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya Afya, Uongozi na Kilimo.
Kwa upande wake Bi. Melinda Gate amempongeza Rais Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya katika kukabiliana na rushwa na kuongeza ukusanyaji wa mapato ya serikali, na pia kwa nia yake thabiti ya kuinua sekta ya kilimo inayotegemewa na idadi kubwa ya watanzania na ameahidi kuwa taasisi ya Bill and Melinda Gates itaendelea kushirikiana na Serikali ya awamu ya tano katika kuongeza tija ya uzalishaji wa mazao ya kilimo.


Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es salaam
29 Juni, 2016