Tuesday, 4 June 2013

JAPANI KUGAWA DOLA 32 BILLIONI AFRIKA

Misaada hiyo ina nia ya kuboresha mazingira ya kukabiliana na kasi ya China.
Waziri Mkuu wa Japani, Shinzo Abe ameahidi kutoa msaada wa Dola 32 bilioni kwa Afrika katika kipindi cha miaka mitano kusaidia ukuaji wa uchumi kupitia sekta za serikali na binafsi. 

Abe ametoa ahadi ya masaada huo wakati wa ufunguzi wa mkutano wa kimataifa wa siku tatu kuhusu maendeleo ya Afrika unaofanyika katika Mji wa Yokohama nchini Japani.
 
Msaada huo unajumuisha utoaji wa Yeni 650 bilioni kwa ajili ya mikopo katika ujenzi wa miundombinu na mpango wa mafunzo kwa ajili ya vijana wa Afrika.
 
 
Abe alisema kuendeleza rasilimali ya nguvu kazi, huduma muhimu za matibabu na kukuza sekta ya kilimo ni mambo muhimu katika kuchochea ukuaji wa uchumi wa Afrika.
 
Alisema kile inachokihitaji Afrika ni uwekezaji katika sekta binafsi ambapo ushirikiano kati ya sekta za umma na binafsi utatoa fursa ya kufaidikia na uwekezaji huo.
 
Tangazo lake hilo linaonyesha shauku ya Japani kuchuana na China katika kuipatia msaada na kuwekeza Afrika, bara lenye utajiri wa maliasili.
 
Licha ya uhusiano wa muda mrefu uliopo kati ya Japani na Afrika, umuhimu wa Japan kwa bara hilo umekuwa ukipungua kulinganishwa na ule wa China ambapo kiwango chake cha biashara na Afrika ikilinganishwa na Japan ni mara tano zaidi na mara nane zaidi katika uwekezaji wa moja kwa moja.
 
China huwa haitangazi kiwango cha msaada wake wa maendeleo lakini ripoti zinadokeza kwamba hutoa hadi dola bilioni mbili kila mwaka.
 
Kiwango ilichotangaza Japani Jumamosi kimepita sana kiwango hicho cha China.
 
Uhusiano wa Japani kwa Afrika unatofautiana na mataifa mengine kwa bara hilo, alisema Abe katika kauli inayoonekana kuikusudia China

Mpango huo utawapa fursa vijana 1,000 wa Kiafrika kujifunza katika vyuo vikuu vya Japani na kujifunza kazi katika kampuni za Kijapani.

No comments: