Thursday, 30 July 2015

Yanga imekatwa



https://encrypted-tbn3.gstatic.com/images?q=tbn:ANd9GcQbUuTEj9npUbzem_59rcZtLFA4-SAVEIKryq-XNDzQ3JvWoDiR

Beki wa Yanga, Juma Adbul (Kushoto) akimzuia winga wa Azam, Farid Mussa wakati wa mechi ya robo fainali ya mashindano ya Kombe la Kagame iliyofanyika kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Azam ilishinda kwa penalti 5-3. Picha na Said Khamis. 
Kwa ufupi
Yanga imetolewa kwenye michuano ya Kombe la Kagame na timu ya Azam kwa mikwaju 5-3 ya penati.
Dar es Salaam. Azam imezima ndoto ya Yanga ya kutwaa taji la sita la mashindano ya Kombe la Kagame baada ya kuitoa kwa penalti 5-3 katika  mchezo wa robo fainali uliofanyika jana kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Baada ya timu hizo kumaliza dakika 90, bila ya kufungana ndipo ilipokuja changamoto ya mikwaju ya penalti ambayo mwaka huu imekuwa mwiba mchungu kwa Yanga ambayo kabla ya penalti za jana tayari ilishakosa penalti tatu katika michezo ya hatua za makundi.
Shujaa wa Azam katika mchezo wa jana alikuwa ni kipa Aishi Manula aliyechaguliwa mchezaji bora wa mechi baada ya kudaka penalti ya tatu ya Yanga iliyopigwa na Haji Mwinyi.
Azam iliyoanza kupiga penalti ilipata penalti zake zote tano zilizopigwa na Kipre Tchetche, John Bocco, Himid Mao, Pascal  Wawa na Aggrey Morris wakati kwa upande wa Yanga waliopata ni Salum  Telela, Nadir Haroub na Godfrey Mwashiuya huku Mwinyi akikosa.
Akizungumzia mchezo huo kocha wa Yanga, Hans Pluijm alisema ameumia kupoteza mchezo huo ambao kwake ulikuwa kama fainali.
“Kupoteza mchezo huu ni pigo kwangu, kwa sababu tulikuwa na malengo ya kutwaa ubingwa katika ardhi ya nyumbani.”
Pluijm alisema,“Kipindi cha kwanza hatukucheza vizuri, japo kipindi cha pili tulitengeneza nafasi nyingi zaidi, lakini mashuti yetu mengi hayakulenga goli.
“Sasa nguvu zetu tunaelekeza katika maandalizi yetu ya ligi inayokaribia kuanza hivi karibuni,” alisema Mdachi huyo.
Kwa ushindi huo sasa Azam itacheza nusu fainali Ijumaa na KCCA ukiwa kama marudiano ya mchezo wa Kundi C ambao Azam walishinda 1-0.
Katika mchezo wa jana timu hizo zilianza mchezo kwa kasi na kushambulia mfulululizo tangu dakika ya kwanza ambapo Azam ilikosa bao baada ya krosi ya Shomari Kapombe kuwapita mabeki wa Yanga, lakini John Bocco alishindwa kufunga.
Yanga ilijibu mapigo dakika moja baadaye kupitia mshambuliaji wake Donald Ngoma aliyewatoka mabeki wa Azam na kupiga shuti lililopanguliwa na kipa  Aishi Manula na kuwa kona ambayo haikuzaa matunda.
Kipa wa Azam, Manula alilazimika kufanya kazi ya kupangua shuti la Juma Abdul alililopiga akiwa umbali wa mita 18 katika dakika ya 8.  Pia mpira wa kurushwa wa Mbuyu Twite nusuru uingie golini kama si ustadi wa Manula kuutoa nje. 
Yanga iliyokuwa ikitumia mfumo wa 4-2-3-1 ambao ni mabeki wanne wakisaidiwa na viungo wawili wakabaji, viungo watatu washambuliaji na mshambuliaji mmoja, ilifanya mashambulizi mengi kipindi cha pili.
Azam iliyokuwa ikitumia mfumo wa 4-3-3, ambao ilitumia mabeki wanne, viungo watatu na washambuliaji watatu, ilitumia mashambulizi  ya kushtukiza na katika dakika 34 nusura ipate bao, lakini shuti la Tchetche lilipanguliwa na kipa wa Yanga, Mustapha ‘Barthez’ na kurudi uwanjani na kumkuta Himid Mao aliyepiga shuti la chini na Tchetche alipojaribu kuunganisha mpira ulipaa juu.
Tofauti na michezo iliyopita, jana washambuliaji wa Yanga, Tambwe,  Ngoma, Mwashiuya na Kaseke walikuwa kwenye wakati ngumu mbele ya ngome ya Azam iliyoongozwa na Wawa, Morris, Kapombe na Kheri  Abdallah iliyocheza kwa maelewano makubwa kuziba njia.
Kipindi cha pili kocha wa Azam, Stewart Hall aliwapumzisha Frank Domayo, na Kheri Abdallah na kuwaingiza Ame Ally na Said Morad wakati Hans Pluijm aliwatoa Kaseke, Juma Abdul, Niyonzima na kuwaingiza Salum Telela, Joseph Zutah na Malimi Busugu.
Pamoja na mabadiliko hayo bado timu hizo ziliendelea kutengeneza nafasi nyingi za kufunga, lakini hakuna timu iliyofanikiwa kutumia na mchezo ukaingia katika ubabe wa hapa na pale.
Twite alinusurika kupewa kadi nyekundu katika dakika ya 74 baada ya kumchezea vibaya Himid Mao wakati akiwa tayari na kadi ya njano aliyopewa dakika 71 kwa kumchezea vibaya Mao. Pia Jean-Baptiste Mugiraneza alipewa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Tambwe dakika 78.
Hadi filimbi ya mwisho inapigwa kuashiria kumalizika kwa mechi hiyo, Azam ilikuwa imetunza rekodi yake ya kutofungwa bao lolote hadi sasa katika mashindano hayo, wakati Yanga ikiwa imefungwa mabao mawili.
Awali KCCA ya Uganda ilijihakikishia kucheza nusu fainali baada ya kuichapa Al Shandy ya Sudan kwa mabao 3-0 kwenye Uwanja huo.
Mabao ya Joseph Ochaya, Muzamir Mutyaba na Tom Masiko yalitosha kuihakikishia KCCA kufuzu kwa nusu fainali kwa mara ya pili mfulululizo.
 Mabingwa hao wa 1978 ni mara ya kwanza katika mashindano ya mwaka huu kufanikiwa kufunga mabao matatu kwani katika mechi zake tatu zilizopita ilifunga mabao mawili tu

No comments: