KUNA
wanaodhani kwamba ujamaa na kujitegemea kama sera ya kiuchumi na kuendeleza
watu vijijini ni kitu kilichoshindikana na kwamba kimepitwa na wakati.
Hata
hivyo, hadi wa leo hakuna kiongozi au msomi aliyekuja na siasa au sera mbadala
vinavyoeleza nadharia na vitendo vipi vitumike, ili kuviondoa vijiji kwenye
lindi la umaskini na kuliingiza kwenye zama za shiibe na wingi wa neema.
Pamoja na hayo, tafiti mbalimbali za watafiti na waandishi wa ndani na nje, sasa zimeanza kudhihirisha kwamba kushindwa kutekelezeka kwa siasa za ujamaa na kujitegemea nchini Tanzania, hivyo vijiji kuhukumiwa kubaki katika umaskini wa kutisha, usiopata msaada wowote wa maana kutoka Serikali kuu na wanasiasa, wakati huko Uyahudi sera kama hizo zimetumika na kuufanya mfumo na muundo wa kibuttz kuwa kitu cha kujivunia kwa kila Myahudi, kulitokana zaidi na ubinafsi wa wanasiasa na hususan viongozi.
Uoga huo kwamba ujamaa na kujitegemea, ushirikishwaji watu na watu kuchangia maendeleo yao wenyewe kuna uwezo mkubwa wa kuwapa nguvu zaidi wanavijiji, hivyo kuwatoa ujingani na kuwaweke katika nuru, ambayo itasababisha wasitawalike, wasinunuliwe, wasigawanyike na wasihadaike kirahisi ni jambo linaloendelea hadi leo.
“ Kuna imani ya kwamba wananchi wa vijijini wakiendelea kuwa masikini, basi watawala wetu fulani wataendelea kutawala milele. Umaskini kwao umegeuka mtaji, tena mara mbili”.
Kwanza,
kujihadaa kuwa wataendelea kupendwa na wanavijiji waamini kuwa wao tu ndiyo
wakombozi na pili, wao kuzila fedha za misaada kwa masikini na umaskini ziku
zote ukabaki palepale au kuongezeka zaidi.
Hatua
ya chini kabisa katika ushirikishwaji watu katika uamuzi na utekelezaji wa
mipango inayohusu maendeleo yao, inaitwa uanasesere au kuchezewa
(manipulation). Katika hatua hii, wale wanaoshikilia madaraka au wenye nguvu na
sauti katika nchi kwa heri au shari, huutumia ushirikishwaji watu kama mbinu
ya uenezi habari na ujengaji mahusiano na watu kwa dhati au kwa unafiki.
Katika hatua hii, watu watakusanywa au wataunganishwa pamoja; wakaahidiwa hiki au kile; wakati mwingine wakitolewa kwenye rutuba na kupelekwa jangwani, wakatoka kwenye neema na kuwekwa kwenye dhiki na kisha mwisho wa yote wale waliowapelekea huko wasiwape uongozi wala msaada wowote wa maana.
Ni katika hatua hii ambayo tunaona badala ya
viongozi kwenda kuishi, kukaa na kupanga pamoja na wananchi ushirikishwaji wao
mia kwa mia, wanasiasa mbalimbali na viongozi kwa ujumla huenda kuwaona
wanavijiji kama vile wanavyokwenda kutembelea wanyama kwenye mbuga za utaliii.
Kufika na kuondoka kwao hakubadili chochote zaidi ya kuwepo mabaki ya pilau,
vinywaji na mapambo ya wao kufika na kuondoka.
Pamoja
na kujulikana kwamba watu wote wanastahili kuwa na mahitaji ya msingi kwa
kusaidiwa na jamii kubwa, yaani, kila familia kuwa na nyumba, shamba,
elimu na mafunzo, afya na tiba, huduma mbalimbali za kijamii, ajira kwa wenye
umri wa kuajiriwa, fursa mbalimbali za kijamii na kiuchumi, wanasiasa huingia
katika wakaligeuza zoezi zima kuwa ni sanaa na usanii mtupu.
Hatua
ya pili ya ushirikishwaji watu ni TIBA. Katika hatua hii maadili, desturi,
imani na mitazamo ya wasiokuwa na nguvu na wasiokuwa nacho hufinyangwa na
kuingizwa ndani ya utamdauni na mila za wale wenye nguvu na uwezo katika jamii
husika.
Katka
mbuga za wanyama au pembezoni ya migodi ya madini, ambayo wakazi wa maeneo
husika walistahili kuwa wanahisa na wamiliki wa miradi inayozuliwa huko,
watu watafungwa macho kwa kujengewa zahanati, shule, kibarabara au
kidaraja na hapo ndiyo ufadhili wa hao wanaovua utajiri wetu kwa mabomba kila
siku ukawa umeishia.
Hadi kufikia hapa, mwananchi mara nyingi anakuwa haijui Katiba ya nchi; hajui haki zake; hajui wajibu wake wala fursa za uteuzi mbalimbali zilizoko mbele yake. Hili linasahihishwa na hatua ya nne, ambayo inaitwa KUTAARIFIWA . Angalau, sasa katika kutaarifiwa mwanakijiji anaweza kujuaa haki, wajibu na fursa alizonazo kijamii na kimaendeleo. Hii ni hatua ya mwanzo kabisa, katika ushirikishwaji kiukweli kweli watu katika uamuzi na utekelezaji wa mipango ya maendeleo na masuala mengine yanayogusa maisha yao ya kila siku.
Hatua
ya USHAURI kwa maana ya kwamba na yeye anakuwa ni mshiriki katika mazungumzo au
mikutano inayohusu maendeleo yake na wanakijiji wenzake, huwa inazidi kumpeleka
juu zaidi mwanakijiji kuwa na nguvu na sauti katika kile kinachofanyika katika
jamii yake. Hapa anasikiliza ujumbe na mawazo ya viongozi au wabia wengine,
lakini pia na yeye anapata fursa ya kuchangia, kukosoa, kuongezea au kukataa
wazo fulani dhahiri bin shayiri.
Hatua
ya KUTAFADHALISHWA kama neno lenyewe linavyojidhihirisha hufikia pale ambapo
hakuna uamuzi wowote, achilia mbali utekelezaji wa jambo lolote hufanyika
pasipo wanakijiji kuliridhia kwa umoja wao. Mathalani, wakazi wa Mkoa wa Mtwara
hivi sasa wanapinga gesi kutoka Mtwara na kupelekwa Dar es Salaam, mabomba Dar
es salaam. Wanataaluma wa ushirikishwaji umma wakihusishwa wanaweza kurejelea
hatua zilizotangulia wakasahihisha na baada ya Wamtwara kushirikishwa na wao
wenyewe wakaona faida au manufaa moja, mbili, tatu watakayoyapata na wabia
wengine wakawatafadhalisha basi wanaweza kuridhia na tatizo hili likawa
limepatiwa ufumbuzi wa muda. Nguvu na kujua sana kukitumika matokeo yake
yanaweza yasiwe mazuri kwa Wamtwara na Taifa kiujumla.
Hatua
ya sita ni UBIA, ambayo kwa kawaida inahusu wenye mamlaka au nguvu kupatana na
wanakijiji au wananchi juu ya jambo fulani,hivyo kwa kiasi fulani watawala
kuwaachia nguvu na mamlaka fulani wanakijiji au wananchi. Mgawanyo huu wa
mwanzo wa mamlaka, lazima uwepo ili kuwawezesha wananchi siyo tu kuwa na kauli
katika uamuzi bali kuanza kutafiti na kuchunguza kisha kuasisi njia mbalimbali
zinazoweza kuwawezesha kuwa na mtaji wa kijamii, jambo ambalo ni muhimu katika
maendeleo ya watu vijijini.
Aghalabu,
mifano mingi inaonyesha kwamba wananchi wakishaanza kushiriki kwenye kufanza
maamuzi na utekelezaji mipango basi hatua ya saba, yaani, KUKAIMU MAMLAKA AU
NGUVU ZA KIUTAWALA, hufikiwa fumba na kufumbua. Ni katika hatua hii,
ambapo wengi wa wanavijiji huanza kujisikia kweli ni watu huru na wanaoweza
kuamua mwelekeo wa maisha yao na siyo kama kule nyuma ambako huwaachia watu
wengine kuamua jinsi maisha yao ya leo na kesho yatakavyokuwa.
Hatua
ya nane UDHIBITI MAMLAKA AU NGUVU na wananchi wenyewe ndiyo hatua ya juu au
kilele katika ngazi ya ushirikishwaji watu katika uamuzi na utekelezaji mipango
yao ya maendeleo. Ili ushirikishwaji wa kweli uwepo vijijini ipo haja ya
kuangalia ni kwa namna gani uongozi wa vijijini unaweza kuanzishiwa muundo na
mfumo utakaorahisisha viongozi hao kupatiwa elimu na mafunzo huko huko vijijini
wanakoishi na kufanya kazi zao. Serikali, mashirika yasiyo ya kiserikali na
sekta binafsi zina mchango mkubwa kwa kuifanya kauli ya 'elimu ni mama wa kila
kitu' kuwa ya kweli vijijini kwa kusaidia na kuwaunga mkono wale wote ambao
kutokana na kazi au shughuli zao za kielimu zinawalazimisha kwa njia moja au
nyingine kuanza kuwaamsha watu na kuwatia mori wa kutafuta elimu na maarifa
mapya ili wabadili maisha yao.
Yaliyozungumzwa
hapa siyo mageni. Yapo katika kumbukumbu za mikutano kati ya Benki ya Dunia na
JMT; kumbukumbu za Azimio la Arusha; kumbukumbu za Vijiji vya Ujamaa Tanzania;
na kumbukumbu za Madaraka Mikoani kama zilivyoandikwa kwa kutumia maandiko ya
watu na taasisi mbalimbali ikiwemo Benki ya Dunia, IMF na Mwalimu Nyerere.
Kilicho tofauti kwa wakati huu ni nyakati kubadilika lakini haja ya kufanya na
kutekeleza hatua za msingi ili kuwa na dhati ya kuupunguza umaskini inabakia
palepale.
Hii
ina maana kwamba, ninachokihubiri hapa ni kwamba haitawezakana
kamwe kwa Tanzania kuondoa umaskini vijijini bila ya wanavijiji kukubali umoja,
kujitolea na kujitegemea kwa maendeleo yao; bila Serikali kuwawezesha wananchi
kwa wananchi hao kunufaika na ardhi yao na maliasili nyingine za nchi. Bila ya
Serikali kurahisisha wananchi kufikia hatua ya juu kabisa katika ngazi ya
ushirikishwaji watu katika uamuzi na utekelezaji mipango yao ya maendeleo huko
huko waliko iwe ni ngazi ya kijiji, kata, tarafa, wilaya au mkoa.
Moyo
wa kujitolea, umoja na ujamaa, kwa maana ya wanavijiji kuishi kama ndugu na
kufaana wakati wa shida na matatizo, kujitegemea na kutumia nguvu za wanavijiji
wote wanaojiweza kupata ufumbuzi wa matatizo ya kiuchumi, kuzalishaji, kijamii
na kimazingira bado ni sera na siasa inayohitjaika na iliyo na nafasi ya kuleta
maendeleo vijijini kwa haraka kuliko njia nyingine yoyote.
Source: Mwananchi Communication